Thursday, 6 April 2017

Utii ni bora kuliko sadaka



Habari msomaji wangu,

Karibu kwenye somo la leo.
Tunasoma kutoka kitabu cha Yeremia 34 kinachoongelea jinsi Mungu mwenyenzi alipoongea na nabii Yeremia na kumpa maagizo yake ili awaambie watu wa Yuda wakaao Israeli nini Mungu anapenda wafanye.

Lakini ukiendelea kusoma unaona jinsi wana wa Yuda hawakutaka kutii maagizo ya Mungu bali kufuata mambo ambayo waliyapokea kutoka kwa mababu zao. Hayo mambo  waliyapenda na kuyaamini kuwa yanawasaidia na hivyo kupelekea hasira ya Mungu kuwaka katikati yao na wao kupelekwa utumwani Babeli.

Mungu akawaambia nitawapa uhuru wa kuteswa na mataifa utumwani. Kumbe Yuda walikuwa na ulinzi wa kimungu juu yao ya kuweza kuzuia watu wasiwatese au kuwaonea. Lakini Mungu akaiondoa wakabaki wenyewe bila ulinzi na hivyo wakateseka kwa mapigo mbalimbali.

Je wewe unateseka na mambo gani katika maisha yako? Umewahi kujiuliza kama bado una ulinzi wa kimungu au umeshatoweka? Mara nyingi kukataa maagizo ya Mungu kunapelekea kuondolewa ulinzi katika maeneo ya maisha yako. Unatakiwa kujichunguza na kujihoji kama unafuata kwa uaminifu maagizo yote yaliyoagizwa kwenye neno la Mungu.

Vitu tunavyoagizwa na Mungu kupitia neno lake ni  kupendana, kusameheana, kuinuana, kutoa zaka na sadaka mbalimbali, kusaidia wasiojiweza, kumsifu na kumuabudu, kuishi maisha matakatifu nk.
Ni vizuri kuyafanya haya yote kwa uaminifu. Mtumie Roho mtakatifu nae atakuwezesha kufanya haya. Pia jitahidi kusoma neno la Mungu kwani ndilo uzima na litakuwezesha kujua nini cha kufanya na kwa namna gani. Kumbuka hakuna kinachoshindikana kwa Bwana kama ukiamua na kuamini.

Utii ni Bora kuliko sadaka, kwahiyo nivema ukatii maagizo ya Mungu na hapo ndipo utakapokua chini ya ulinzi wa Mungu katika kuingia kwako na kutoka kwako, na shetani hatapata nafasi katika maisha yako.

Matatizo mengi huja kwa kuachwa mlango wazi katika maisha yako. Funga milango yako yote ili shetani asipate nafasi. Funga milango ya uongo, uvivu, wivu, masengenyo, ulafi, uzinzi, ufisadi, kuabudu/kutegemea miungu mingine n.k. uone kama utaonewa tena na shetani. Hakika hatapata nafasi.

Usiwe kama wana wa Israeli ambao hawakutii maagizo ya Mungu, na mabaya yakawapata. Anza kutii maagizo ya Mungu leo uishi katika ulinzi wake.

1 comment: