Friday, 31 March 2017

Unaweza kupata unachokitaka kutoka kwa Mungu



Habari msomaji wangu,
Karibu kwenye somo la leo.

Tunamtumikia Mungu mkuu na mwenye upendo. Ni maombi yangu kwako kuwa wewe na wale wote wanaokuzunguka muweze kujua na kuishi upendo wa Mungu na ukuu wake kwa kiasi kikubwa kuliko hapo mwanzo.

Lakini ngoja nikuulize kitu: Je unayo imani ya kuweza kuamini mambo makuu ya Mungu katika maisha yako?

Neno la Mungu linasema Mungu yuko kwa ajili ya kukuongeza na kukufanya usonge mbele, Mungu huwa harudi nyuma. Tunasoma kwenye Hagai 2:9,  “Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza.”  Hii  ina maana kuwa Mungu hayuko katika kurudia kitu alicho kifanya bali kufanya vizuri zaidi na kwa upya, na ataenda kufanya kitu kikubwa zaidi kwako Haleluya!

Yesu alisema wale wote watakaomuamini watafanya mambo makubwa zaidi ya yale aliyoyafanya yeye Yesu (Yohana 14:12).

Nimegundua ya kuwa imani na matarajio yanakwenda pamoja. Kama mtu anasema anayo imani juu ya kitu fulani halafu mwenendo wake hauonekani kukitarajia hicho kitu kutokea, hiyo inakuwa ni kama kufikirika tu (wish) na siyo imani.

Natamani kwa ujumbe huu ukaimarishe imani yako ambayo itazaa matarajio katika maisha yako ili kuona na kuishi mambo makubwa ambayo Mungu wetu anayo kwa ajili ya maisha yako.

Je unaamani kabisa kuwa Mungu anacho kitu kizuri na kikubwa kwa ajili ya kazi yako, ndoa yako, watoto wako fedha zako, utumishi wako na mambo yote katika maisha yako? Kama ndiyo, basi tarajia kuwa itakuja kuwa halisi katika maisha yako.
Yesu alisema “ Je unaamini ya kuwa ninaweza kukufanyia haya?..... Kutokana na imani yako pokea “ ( Mathayo 9:28-29).

Imani na matarajio huenda pamoja. Ila haitaishia hapo. Kama kweli unaamini, na unajua itakuja kutokea, basi tutaona kwa namna unavyoongea na kuishi

Najua kuna watu ambao wanafikiri kusema au kukiri kitu hakina uhusiano na kupokea hicho kitu. Kama ukitamka na kuweka maneno unayotamka katika imani na matarajio, utakuwa unatengeneza mazingira ya Mungu kukufanyia au kukupa hicho kitu katika maisha yako, na tena kwa haraka zaidi kama hutakata tamaa. Hii ndiyo njia ya kibiblia ya kupata vitu vyako unavyovihitaji.

Kuna laana na uzima katika kuongea (Mithali 18:21). Unaweza ukaona hili neno likifanya kazi kuanzia agano la kale, agano jipya na hata katika maisha yetu ya kawaida.

Mtume Paulo anatuambia kwenye Warumi 4:17 yakuwa Mungu alimuita Abram kuwa Abraham kwasababu yeye atakuwa Baba wa Mataifa mengi. Hapa tunaona Mungu alimuita Abraham baba wa mataifa mengi wakati Abraham alikuwa hana hata mtoto mmoja, na mke wake Sara alikuwa tasa na mwenye umri mkubwa. Embu angalia mazingira aliyokuwa nayo Abraham na mkewe yalikuwa ni magumu kwa macho ya kibinadamu. Ni kitu ambacho hakiwezekani lakini Mungu aliamua kutamka hivyohivyo.

Je wewe uko na mazingira gani ambayo unaona magumu na haiwezeni kupata unachokitamani? Embu amua kutamka na kuamini ya kuwa kitawezekana leo na uanze kukiishi hatakama hakijatokea bado haleluya! Kwasababu tumeambiwa kwa kadiri ya imani yetu tutapokea kutoka kwa Mungu.
Tunaona nguvu ya kutamka kitu unachokihitaji ni muhimu sana. Na siyo kutamka mara moja tu, fanya hivyo kila siku. Na ukitaka iwe rahisi kwako kufanya hivyo, hakikisha unachapa hilo hitaji lako kwenye karatasi au andika kwa mkono kwenye karatasi, halafu ibandike kwenye ukuta wako wa chumbani,  ofisini, kwenye computer yako kwenye wallet yako nk. Hii itakusaidia ukiwa popote unaweza kuisoma na inakukumbusha kuwa unakitu unakitarajia kutoka kwa Bwana.
Tumeona hapo kwenye warumi 4:17. Mungu alikuwa anatamani kuona Abraham akiwa ni baba wa mataifa mengi. Mungu hakuishia kutamani tu, bali alianza kuifanyia kazi imani yake kwa njia ya kimatendo kumbadilisha jina Abram kuwa Abraham. Hiki kitendo ndicho kile tunasema kuiishi imani. Yaani unaanza kuanda mazingira ya kupokea muujiza wako.

Mtume Paulo anatuambia tunayo roho ileile ya imani kama Baba yetu wa mbinguni (2 Wakorintho 4:13). Usiruhusu mazingira yako yakufanye uongee unachokiona kwa wakati huo. Anza kusema “mambo makubwa yasiyoonekana yanakwenda kutokea katika maisha yangu, Baraka za Mungu, na kufunguliwa kwangu kunakwenda kutokea”.
Hivi ndivyo  ninafanya katika maisha yangu na ninaona mambo makubwa yakinitokea pale ambapo palikuwa panaonekana haiwezekani kabisa, naona Mungu akifanya.   

Kila mara ninapokwenda kusikiliza neno la Mungu natafuta ni nini Mungu anasema na ninalichukua na kulifanya la kwangu na kuanza kulitamkia na kuliishi kana kwamba nimelipata tayari. Na ndipo hilo neno huwa halisi katika maisha yangu.
Kuna ujumbe mwingi sana ambao wewe kama mkristo unaupata kwa kuhudhuria semina na makongamano mbalimbali na huko kote Mungu anakuwa na ujumbe mahususi kwa ajili ya tatizo au hitaji ulilonalo. Shida inakuwa ni pale hauko tayari kutafuta nini Mungu anasema nawewe ili uuchukue na kufanyia kazi kama nilivyoelezea. Mara nyingi unasifia tu ujumbe ni mzuri lakini wewe huchukui hatua ya kuufanya ujumbe uwe wa kwako na kuunenea kila siku na kuishi kama vile umeshakuwa halisi.

Mpendwa msomaji wangu. Tunaambiwa ya kuwa tunaangamia kwa kukosa maarifa. Embu pata maarifa leo na uanze kubadilisha maisha yako. Chukua hili kama desa lako. Copy na upaste kwenye maisha yako na uone jinsi utakavyo anza kuishi kwa ubora zaidi kuliko hapo mwanzo.

Sunday, 26 March 2017

Unaweza Kuishinda Dhambi

Habari za leo mpendwa msomaji wangu. 
Karibu kwenye somo hili la namna ya kuishinda dhambi.

Watu wengi wanajiuliza ni kwa namna gani mtu anaweza kuishinda dhambi akiwa hapa duniani. Embu tuangalie Waefeso 2:1-10 inasema:
"Ninyi mlikuwa mmekufa kwa sababu ya makosa na dhambi zenu. Wakati ule mliishi kufuatana na mtindo mbaya wa ulimwengu huu, mkawa mnamtii mtawala wa pepo wenye nguvu wa anga, pepo ambao huwatawala sasa watu wasiomtii Mungu. Na hata sisi sote tulikuwa kama wao; tuliishi kufuatana na tamaa zetu za kidunia na kufanya tu mambo yale yaliyoipendeza miili na akili zetu. Kidunia, sisi kama vile pia wao, tulistahili ghadhabu ya Mungu.  Lakini Mungu ni mwenye huruma nyingi. Alitupenda kwa mapendo yasiyopimika,  hata, ingawa tulikuwa tumekufa kwa sababu ya dhambi, alitufanya hai pamoja na Kristo. Kwa neema ya Mungu ninyi mmeokolewa.  Kwa kuungana na Kristo Yesu, Mungu alitufufua pamoja naye, tukatawale pamoja naye mbinguni.  Ndivyo alivyopenda kuonyesha kwa watu wa nyakati za baadaye, ukuu wa neema yake aliyotujalia kwa ukarimu katika kuungana kwetu na Kristo Yesu."

Hapa tunaona kuwa kwa kitendo cha kuungana na Yesu Kristo yaani kumpokea Yesu katika maisha yako na moyo wako, unaweza kupata neema kwa Mungu ya kukufanya hai tena pamoja na Kristo wakati ulikuwa umekufa kwasababu ya dhambi zako. Kwahiyo sasa umefufuliwa na Yesu Kristo ili ukatawale nae mbinguni.

Cha kujiuliza hapa nikuwa unawezaje kutawala na Yesu mbinguni wakati unaishi bado katika maisha ya dhambi? Neno la Mungu linasema katika Ufunuo 21:27 hakuna kinyonge kitakachoingia mbinguni na kuna sehemu nyingine inasema Mungu hupendezwa na watakatifu walioko duniani. Je unataka kuwa mtakatifu wewe hapa hapa duniani? Je ni kwa namna gani unaweza kufanikiwa kuacha dhambi.

Tunajua ya kuwa Mungu wetu ni mtakatifu, nae hukaa mahali patakatifu yaani ndani ya moyo wako. Ili uweze kushirikiana na huyu Mungu mtakatifu, inakubidi na wewe uwe mtakatifu na kuishi maisha matakatifu.

Unaweza kuwa mtakatifu kama utaamua. Kumbe tunaona UAMUZI wako ni kitu muhimu sana katika wewe kuweza kuishi maisha matakatifu au la.

Je ni kwa namna gani?
Ili kuweza kuacha kabisa dhambi unatakiwa uamue kufanya hivyo. Amua toka ndani ya moyo wako kuwa dhambi ni uasi kwa Mungu na kuwa inamchukiza Mungu. Pia utambue kuwa kwa kufanya dhambi unaweza usipate muda wa kutubu na ikakupelekea kwenda motoni. Ukiisha kukaa na kutafakari ndani yako kwa habari ya madhara ya dhambi yoyote ile iwe ni kubwa au ndogo, ndipo utakapopata majibu ya namna gani uichukulie dhambi.

Neno la Mungu linatuambia tuchague kumpenda Mungu na kuachana na dhambi ili tupate uzima wa milele. Sema hapana kwa dhambi yoyote hata kama inakufurahisha kwa namna gani. Fikiria kuwa hiyo raha au starehe unayoipata sasa hivi kwa kuifanya hiyo dhambi itageuka uchungu wakati ujao na utajutia.

Ni kwa jinsi gani unaweza ukawa na uamuzi unaofaa?

Ni kwa kuanza kuwaza mwisho wako (future) unaotaka uweje. Ukishakuwa na picha ya mwisho wako au future yako, ni rahisi kuweza kupangua vitu ambavyo vinaweza kukwamisha katika kuufikilia huo mwisho mwema unaoutarajia.

Mfano, unataka kuingia mbinguni na kumuona Mungu mwisho wa maisha yako. Na unakutana na mtu anakuambia nakupenda twende tukazini japo kidogo tu. Kitu cha kwanza unachotakiwa kufanya ni kuufikiria au kujikumbusha ule mwisho wako ni nini halafu rudisha mawazo yako katika hicho kitu ambacho hata wewe mwenyewe unakitaka kukifanya kwa saa hiyo, halafu jiulize je kwa kufanya hiki kitendo naweza kuhatarisha maisha  au kuyaendeleza maisha. Ukishapata jibu kuwa unaweza kuhatarisha  kwasababu huenda unaweza ukafa ukiwa katikati ya hilo tendo au Yesu akarudi ukiwa katikati ya hilo tendo. 
Ukishaweza kupata jibu la hapana sitafanya ni lazima uanze kufikiria namna ya kuondoka au kukaa mbali na hilo jambo, au huyo mtu au hiyo sehemu nk. 

Biblia inatuambia tuikimbie dhambi kama Yusuphu alivyoikimbia dhambi hii kutoka kwa yule mke wa farao.

Uzuri ni kwamba kila wakati ukichagua kufanya uamuzi sahihi, hatimaye Roho mtakatifu anakusaidia kuondoa tamaa ya hicho kitu ndani yako na unaanza kuwa HURU kabisa mbali na hiyo dhambi. Na hii ni kwa watu wote wanaume na wanawake, watoto, vijana na wazee. 

Mpendwa msomaji wangu. Ninajua kuwa hili somo si rahisi sana kama tunavyoongea, lakini kwa msaada wa Mungu na Roho Mtakatifu tunaweza tukashinda dhambi kabisa na kuwa huru kama vile Mungu anavyosema Watakatifu walioko duniani ndiyo ninaopendezwa nao.

Kumbuka dhambi moja ni mlango wa kuleta dhambi nyingine. Anza leo KUAMUA kuachana na hiyo dhambi inayokusumbua kila wakati na kuitubia kila wakati  uone utakavyokuwa huru na kuishinda kabisa. "INAWEZEKANA KUWA HURU MBALI NA DHAMBI"

Monday, 20 March 2017

Ukame Umekwisha

Mpendwa msomaji wangu,
Ili kuweza kupenyeza katika ukweli wa kuishi kiuhalisia wa maisha ya kiroho (supernatural living) unahitaji uwe kama mtu aliye "mpumbavu" hivi.
1Wakorintho 1:27 inasema "Bali Mungu alivichagua vitu vipumbavu vya ulimwengu ili awaaibishe wenye hekima; na Mungu alivichaguwa vitu dhaifu vya ulimwengu ili aviaibishe vitu vyenye nguvu."

Upumbavu hapa haina maana ya ujinga au asiye na akili bali inaongelea wale ambao wanajua wanahitaji huruma na msaada wa Mungu kwasababu bila ya Mungu hawawezi wao wenyewe. Wanajua wana muhitaji Bwana Yesu ili kuweza kuwasaidia kuishi yale maisha ambayo wanayatamani (desire).

Neno la Mungu liko kwa ajili ya kuleta imani moyoni na si kuleta mantiki akilini. Angalia 1 Wakorintho 1:22-23 inasema " Kwa maana Wayahudi wanaomba ishara na Wagiriki wanatafuta hekima. Lakini sisi tunamhubiri Kristo aliyetundikwa mtini, kwa Wayahudi ni sababu ya kujikwaa lakini kwa mataifa ni upumbavu"

Mashindano baina ya akili (intellect) au kujisikia(feelings) na moyo (heart) ambamo imani hukaa inaweza kuonekana pale ambapo watu wanaambiwa wamtolee Mungu fungu la kumi na sadaka mbalimbali. Kama akili yako haijageuzwa na Roho Mtakatifu, basi utashi wa kibinadamu hutawala na mtu huishia kufuata hisia zake za kutokutoa. Mtu wa namna hii anakuwa ni mtu wa Ufalme wa Mungu lakini anaishi chini ya utawala wa dhambi na laana ya dunia.

Fungu la kumi na sadaka nyinginezo ni ahadi ambazo hazikwepeki kwa mtu wa ufalme wa Mungu kuzifanyia kazi kama atataka kupata mpenyo wa kifedha na maisha bora kwa ujumla wa kimwili, kinafsi na kiroho. Namna ambayo Mungu anatupa mahitaji yetu ni kwa kupitia mbegu tunazozitoa.

Ngoja nikupe mfano wa kitu halisi kilichonitokea mimi mwenyewe kwa habari ya kutoa fungu la kumi.

Kama familia kwa wazazi wangu tulikuwa tunadaiwa na benki moja bilioni 2. Sasa ikafika wakati ni lazima tuuze nyumba iliyokuwa na dhamana kwa ajili ya kulipa benki. Tukatafuta wateja kwa muda mrefu sana kama kwa miaka miwili hivi hatukuweza kupata mtu wa kuweza kuinunua. Sasa nikawa najifunza mambo mengi ya namna ya kutoka kimaisha na kuweza kupata ninachohita ji kibiblia. Nikaweza kujifunza pia kwa habari ya utoaji mbalimbali kama neno la Mungu linavyoagiza. Nikawa ninaanza kutoa fungu la kumi kwa hela ndogo nazopata. Baada ya muda nikawa ninafuatilia mafao yangu ambapo nilikuwa nimeacha kuajiriwa na kuingia kujiajiri. Nilivyopokea tu yale mafao nikakumbuka natakiwa nitoe fungu la kumi. Ingawa hela ilikuwa kubwa ya kutoa maana ili kuwa kwenye milioni kadhaa hivi nikajitia moyo na kusema hapa ndipo imani yangu itakapopimwa.
Nikaamua kuitoa na nikaiombea iweze kufungua nyumba yetu iweze kuuzika.
Kesho yake baada ya kutoa hiyo fedha, kuna dalali ambaye hatukuwa tunafanya nae kazi wala hatumjui akaja asubuhi na mapema na kusema nasikia mnapauza hapa na nimekuja na mteja. Kwakweli waliponipigia simu na kuniambia niliona kama ni wale wale tu maana tulishazoea watu kuja na kuyeyuka. Nahapo watu wa nyumbani kwangu hawakujua kama kuna hela nimetoa kama sadaka tena nyingi maana wasinge nielewa.

Lakini yule mteja alikuwa serious na akasema twende mkanitambulishe benki kuwa mimi ndiyo nitanunua. Maana hapo benki walikuwa wametupa wiki mbili tu wao watakuja kuinadi. Basi tukampeleka na akajicomit na kuanza kutoa hiyo hela. Na alipo maliza kulilipa hilo deni akatupatia na sisi hela nyingi tu kwa ajili ya kuendelea na maisha. Kwakweli Mungu ni mkubwa kwasababu nilimuona Mungu amefanya kama alivyosema katika neno lake kwamba hatakawia tusipovunjika mioyo.

Sasa embu tuone tulichojifunza kutokana na ushuhuda huu;
Kwanza, huwezi kupata jaribu lolote kubwa ambalo huwezi kulivuka. 1 Wakorintho 10:13. Katikati ya hitaji nilikubali kufanya kitu ambacho kilimgusa Bwana na mbegu hiyo ikafungua madirisha na kuondoa ukame uliokuwepo.

Pili, Gundua mbegu yako na uwe tayari kuipanada na siyo kuisevu au kuila. Kumbuka, kama ukitoa kilichoko mkononi mwako, na Bwana atatoa kilichoko mkononi mwake kwa ajili yako. Bwana anao Ulimwengu mzima mikononi mwake 1Wafalme 17.

Tatu, Unaweza ukaiamulia mbegu yako ifanye chochote unachokitaka ifanye. Mbegu yako inaweza kuwa chochote kinacho mbariki mtu mwingine.

Nne, Siyo sana ukubwa wa mbegu yenyewe bali ni imani iliyowekwa kwenye hiyo mbegu. Mavuno utakayoyapata ni makubwa mno kuliko mbegu uliyoitoa. Marko 12:43.

Tano, Hakuna janga lolote kubwa litakaloondoa hii kanuni ya kupanda na kuvuna isifanye kazi kwako kama utaizingatia. Hii kanuni itaendelea kufanya kazi na ni ya milele kama usiku na mchana. Mwanzo 8:22, Jeremia 33:19.

Kwahiyo kama utatamani kuondoka kabisa kwenye hiyo hali uliyonayo ya ukame katika maisha yako, anza kufanyia kazi maneno haya niliyokuambia uone kama maisha yako hayatabadilika na kuwa kama unavyo tamani siku zote. INAWEZEKANA!
 
 

Friday, 17 March 2017

PALE ILIPO HAZINA YAKO, NDIPO ILIPO NA MOYO WAKO


Luka 12: 32-34

"Msiogope enyi kundi dogo, maana Baba yenu amependa kuwapeni ufalme. Uzeni mali yenu mkawape maskini hizo fedha. Jifanyieni mifuko isiyochakaa na kujiwekea hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wezi hawakaribii wala nondo hawakaribii. Pale ilipo hazina yako, ndipo pia utakapokuwa moyo wako."

Je  umewahi kujiuliza ni kwanini unapenda sana kitu Fulani au mambo fulani katika maisha? na jambo hilo unalifikiria sana usiku na mchana? Hii ni kwasababu nguvu yako yote ya hali na mali umeielekeza huko. Napia ni kwasababu unajitahidi sana kwa nguvu zako kuhakikisha hicho kitu kinakaa vizuri kama upendavyo na hii ni kwasababu hicho kitu kinathamani sana katika maisha yako.

Biblia inatuambia popote hazina yako ilipo pia moyo wako upo. Ukiona umeconcentrate sana mahali Fulani ujue kuna hazina yako.
Je wewe umeconcentrate zaidi wapi katika maisha yako? Ni upande wa Mungu au wa dunia?

Yesu anatuambia tusiogope kwa maana Baba wa Mbinguni anataka kutupa ufalme. Lakini sharti tujiwekee hazina zetu mbinguni. Kwanini alisema hivyo? Tena akasema mkaviuze mlivyonavyo.
Hii inamaana kuwa tunatakiwa kusalimisha hazina zetu zote kwa Bwana Yesu kwasababu mahali hazina ilipo na moyo huwa hapohapo.

Kama utakuwa unamtegemea Bwana Yesu katika kazi zako zote na kuamini kuwa yeye ndiye msimamizi wa kila jambo basi na moyo wako utamtafakari yeye siku zote na kumpa yeye utukufu katika kila jambo ambalo unalifanya au unalipata.

Watu wengi wanatumia hazina zao kinyume na mapenzi ya Mungu kwa kujifurahisha wenyewe na kwasababu wanatumia kwa maslahi yao, na moyo wao unakuwa hukohuko ambako fedha zao wameweka. Mfano Unamkuta mtu anabadilisha maumbule yake kwa kufanyiwa operesheni ili awe na matako au maziwa mazuri au kiuno kizuri au sura nzuri nk. Hiyo fedha ambayo ni hazina yake ameitumia kujifurahisha mwenyewe na huku akimkosoa Mungu kuwa hakumuumba vizuri hii ni dhambi inayopaswa kutubiwa na kuachwa mara moja. Mtu huyu utakuta kila wakati anajiangalia yeye mwenyewe na moyo wake uko katika kujiangalia kama amependeza au watu wanamuonaje  na hii ni mfano tu wa ilipo hazina yako na moyo wako upo hapo.

Wengine ni wagonjwa, badala ya kumuangalia Kristo na kutafakari njia zake na maneno yake ya uponyaji, wao wanatumia fedha zao na nguvu zao kwenda kwa waganga na ndiko huko  moyo wao unapo kuwa kwasababu wanategemea huko.
Hatakama unatumia dawa za hospitali, unatakiwa kuweka moyo wako kwa Yesu Kristo zaidi kwa kukiri maneno yake ya uponyaji.

Nakusihi ujichunguze kama ni kwa jinsi gani unatumia hazina yako . Unaitumia kwa manufaa yako binafsi au kwa utukufu wa Mungu. Kwasababu hazina na moyo ni vitu vinafuatana pamoja.
Pale hazina yako ilipo na ndipo na moyo wako unapokuwa.