Wednesday, 24 May 2017

Kumwabudu Mungu katika roho na kweli



Yohana 4:23
“Lakini saa inakuja, nayo saa ipo ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katila roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.”

Katika mstari huu tunaweza kuona ya kuwa kuna waabudio halisi. Na kama kuna waabudio halisi pia kutakuwa na waabudio wasio halisi. Pia inasema waabudio halisi ni wachache na ndiyo maana Baba anawatafuta hao ili wamwabudu.

Je ni kwa namna gani unaweza kumwabudu Mungu?

Ni kwa kuishi maisha ya rohoni katika kila nyanja ya maisha yako. Iwe kwa kusema kwako, kwa kutenda kwako na kutembea kwako.
Kuabudu anakokutaka Mungu Baba ni kule kunakotoka katika roho yako na siyo katika nafsi yako. Tofauti ni kuwa, kwenye nafsi yako ndiko kunakotoka kufikiri kwako na kuona mantiki ya kitu kutokana na mazingira yanayokuzunguka, watu wanavyosema au wewe unavyojisikia.

Kwenye roho yako ni mahali ambapo ni pa ukweli unaotokana na neno la Mungu, roho huangalia neno na si mazingira. Ndiyo maana hata ukiwa katika taabu unatakiwa ufurahie kwasababu neno linasema hivyo. Kwenye roho hakuna kikomo ni utimilifu tu na ukiamini na kuishi katika roho, hakika utakuwa ni mtu wa kuishi maisha ya ushindi tu kila siku.

Utajuaje kama unamuabudu Mungu katika roho na kweli au la.

Mtu asiyemwabudu Mungu katika roho anakuwa anaabudu kutokana na mazingira yanayomzunguka. Mfano umefaulu shule ndipo unamuabudu kwasababu hiyo, au unauchungu fulani ndipo unaingia kumuabudu Mungu kutokana na hisia ulizonazo na kulia kwa uchungu.



Mara nyingi hata nyimbo za kuabudu unakuta zinaimbwa lakini maneno yake unakuta yanatuongelea sisi na maisha yetu badala ya kumuongelea Mungu na uweza wake. Kwahiyo unakuta mtu anavuta hisia ya vitu vinavyomzunguka na kupata msisimko akifikiri anamuabudu Mungu kumbe la hasha.

Kumuabudu Mungu katika roho na kweli siyo tukio (event), bali ni maisha ya kila siku na kila wakati. Hii ina maana unamwabudu Mungu kwa jinsi alivyo yeye pekee, uweza wake, ukuu wake, bila kuruhusu akili yako kusikiliza hisia zinazokuzunguka.


Tumuombe Roho Mtakatifu atuwezeshe kumwabudu Mungu katika roho na kweli ambapo tutamuangalia yeye tu na uweza wake pasipo kuangalia magumu yaliyotuzunguka.

Kuwekwa huru mbali na sheria ya dhambi



Warumi 8:1-2
“Sasa basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwasababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru mbali na sheria ya dhambi na mauti.”

Hii ni kwa namna gani?
Kipindi kile cha sheria ya Musa, watu walikuwa wanaishi kutegemea mwili na si rohoni. Mwili ni dhaifu kwa habari ya kufuata sheria za Mungu. Hii ilitokana na laana ya dhambi iliyofanyika pale katika bustani ya Edeni ambapo Eva alidanganywa na nyoka na kula tunda alilokatazwa na Mungu. Walipoondolewa kutoka bustanini, utawala wote waliokuwa nao Adam na Eva uliingia mikononi mwa shetani ambaye ni mleta laana.

Hata sheria ya Mungu iliyoletwa na Musa ilipokuja, kwasababu ya laana, watu  hawakuweza kuitimiza sheria. Watu walibaki wakiwa wanahukumiwa kwasababu ya dhambi zao na kuishi maisha ya kushindwa kila wakati.

Ashukuriwe Mungu mwenyenzi kumleta Yesu Kristo mwanane na kuja kufa kwa ajili yetu na kuondoa sheria ya dhambi na mauti iliyoletwa na shetani, na kuweka sheria ya uzima ndani ya kila atakaye muamini. Ukiamua kumwamini Kristo Yesu, basi hakutakuwa na hukumu ya dhambi na mauti juu yako kwasababu sheria ya roho wa uzima inakuweka huru mbali na sheria ya dhambi na mauti. Na hii inawezekana kwasababu wewe utakuwa hauenendi tena katika mwili ambao ni dhaifu kupokea sheria za Mungu, bali uko katika roho ambamo sheria ya Mungu inawekwa ndani yako automatically, wala hutakuwa na haja ya kutumia nguvu kuacha dhambi. Utajikuta tu unajua hii ni dhambi na hivyo utaachana nayo au utakaa mbali nayo.

Mpendwa msomaji ukiona bado unatumia nguvu sana kuacha dhambi na kwa muda mrefu, nakusihi ujichunguze kwa habari ya wokovu wako kwasababu hutakiwi kuishi na tamaa za mwili wakati unatakiwa kutawaliwa na Roho Mtakatifu ili akuweke huru mbali na dhambi na mauti.

Thursday, 4 May 2017

Namna ya kumlilia Mungu katika shida yako



Zaburi 107:19-20 inasema “Wakamlilia Bwana katika shida zao. Akawaponya na shida zao.Hulituma neno lake huwaponya. Huwatoa katika maangamizi”

Ashukuriwe Mungu aliye juu kwakuwa tunalo tumaini katika yeye. Kwakuwa ndiye ngome yetu na msaada wetu wakati wa mateso.

Leo ningependa nikukumbushe kwa habari ya kumlilia Mungu katika shida uliyonayo.Kwa maana imeandikwa muite Mungu maadamu anapatikana.

Mara nyingi tunakuwa katika shida na taabu katika maisha yetu na tunakaa hapo hapo katika hiyo shida kwa muda mrefu sana kuliko ilivyotakiwa. Ni kwanini? Hii ni kwasababu hatumlilii Mungu katika shida zetu. Unaweza kujiuliza mbona huwa ninaomba sana lakini majibu hayaji. Hii pia ni kwasababu unaomba vibaya. Imeandikwa kuwa” hampati kwasababu mnaomba vibaya”.

Kuomba vibaya ni kwa namna gani?
Ni kwa kulalamika na kuliangalia tatizo lako zaidi ya kumuangalia Mungu na uweza wake wa kuliondoa tatizo. Mara nyingi unakuwa na maombi yanayotokana katika nafsi yako kuliko yanayotoka rohoni. Rohoni ni mahali pasipo na waa na ndipo Mungu hukaa. Kwenye nafsi yako ni mahali unafanya maamuzi kutokana na hali halisi inayokuzunguka. Hivyo kuomba vizuri ni kuomba sawasawa na neno la Mungu, na si mapenzi yako.
Tukiweza kuomba sawasawa na neno lake, atasikia. Mara kwa mara tunaomba sawasawa na mapenzi yetu, na ndipo Mungu hatusikiii kwasabau hujaingia bado kwenye himaya yake. Kulia sana na uchungu sana hausaidii na tena imeandikwa “uchungu wote na uondoke kwenu.”

Embu chunguza hayo unayomuomba Mungu na namna unavyomuomba, je unaomba kwa hisia ya mwilini au katika roho? Mungu ni roho, ukitaka kuongea nae uwe katika roho na ndipo Roho Mtakatifu hutusaidia pale tunaposhindwa kuomba katika roho.

Nakusihi uanze kutafuta kujua namna ya kumuomba Mungu katika roho na utaona jinsi majibu utakavyoyapata kwa haraka kama neno linavyosema walimlilia, wakaponywa na kuondolewa katika maangamizi yao.

Mungu yuko tayari kukupa hitaji lako unalomuomba, ni wewe ambaye unachelewa kujua mapenzi yake ili uweze kupata haja za moyo wako.