Monday, 24 April 2017

Ulimwengu haututambui




Karibu kwenye somo la leo.

1 Yohana 3: 1 inasema “Tazameni ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwasababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye.”

Ni jambo la kushukuru sana kuitwa mtoto wa mtu mkubwa, maarufu na mwenye utajiri mwingi hapa duniani.  Na hii ni kwasababu unajua ya kuwa matatizo  utakayoyapata yatatatuliwa kwa haraka na bila shaka kabisa. Mtu mwenye uwezo wa kifedha na  maarifa ni mtu anayeweza kutatua changamoto zake kwa uraisi zaidi kuliko mtu asiye na fedha na maarifa. Ndiyo maana watoto wa matajiri wanakuwa na hali nzuri zaidi kimaisha kuliko watoto wa masikini.

Tukiangalia neno letu la leo tunaona ya kuwa tumeitwa wana wa Mungu na ndivyo tulivyo kama ilivyoandikwa pia kwenye  Yohana 1: 12 inayosema “ Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika wana wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake;” Wewe kama umempokea Yesu kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako, ujue tayari wewe ni mtoto wa Mungu.

Naomba tumuangalie huyu Mungu wetu alivyo ili tuweze kujua ni kwa namna gani wewe kama mtoto wake unatakiwa kuishi hapa duniani.
Mungu wetu ni mwenye uweza wote, ndiye aliyeziumba mbingu na dunia na vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana. Ndiye mwenye kusamehe dhambi, Mungu ndiye mwenye dhahabu zote na fedha zote. Mungu anawalinzi ambao ni malaika wanaotulinda na kutuletea haja zetu usiku na mchana. Mungu ndiye mwenye kutupa pumzi ya uhai ili tuishi. Mungu hashindwi na lolote. Mungu ndiye mwenye mipango yako yote na ndiye mwenye kujua kila kitu katika maisha yako. Ukiomba chochote kwa Mungu sawasawa na mapenzi yake anakupa.

Mpendwa msomaji wangu, hivi kama huyu ndiye Mungu ambaye ni baba yako na  wewe ni mtoto wake, umesha wahi kujiuliza mbona maisha yako hayafanani na uweza wake?  Huenda tatizo ni sisi wenyewe kwa kutokumjua vizuri Mungu wetu na anataka nini kwetu.
Mara nyingi sisi tulioitwa watoto wa Mungu tunaishi maisha ambayo yanamichanganyo. Kwa Mungu kidogo, na kwa dunia kidogo. Tumeona katika hili neno  ya kuwa dunia haiwatambui wana wa Mungu, kwasababu hawakumtambua Mungu. Hii ina maana gani? Ukiwa kama mwana wa Mungu ni lazima utakuwa tofauti na dunia, kwa kuvaa, muonekano, kuongea na hata namna unavyoishi. Na kwasababu ya tofauti hizo, dunia inashindwa kukuelewa kwasababu vile vitu ambavyo wao wanavikimbilia, wewe huvikimbilii. Kama wewe ni makini wa kufuatilia maneno ya Mungu, utagundua vitu vingi ambavyo vinaendelea duniani ni kutoka kwa yule mwovu.

Tuangalie mfano mmoja wa mavazi, watu wa Mungu ambao ni kanisa lake kuna namna ambayo wanatakiwa kuonekana kama vile wanawake wasivae nguo fupi au wasivae suruale, na pia wasijipambe kwa dhahabu na kusuka nywele za bandia na mapambo ya  usoni (cosmetics). Haya yote yanaitwa ni machukizo mbele ya Mungu ambaye ni baba yetu. Kama wewe bado unafanya mambo kama hayo, ujue unamchukiza baba yako na unafanya mambo ambayo ni ya kidunia na kuacha mpango mzima wa Mungu katika maisha yako.

Mungu wetu anataka tuwe safi bila mawaa katika maisha yetu na siyo michanganyo ambayo mwishowe atakutapika siku zijazo.
Je wewe ni mwana wa Mungu nabado uko katika michanganyo hii ya dunia? Huenda ndiyo maana mambo yako hayaendi na kila ukiomba unaona kama unagonga mwamba. Ondoa unajisi katika maisha yako na uone jinsi Mungu ambaye ni baba yako wa mbinguni atakavyoshuka na kukuhudumia. Usimpe shetani nafasi kwa chochote katika maisha yako.

Soma zaidi maandiko yafuatayo kuhusu namna Mungu anavyopenda uwe na utagundua kumbe ni kinyume kabisa na namna dunia inavyotaka uwe.
1Wakorintho 14:34-35, 1Wakorintho 11:1-15, 1Timothy 2: 8-15, 1 Petro 3:3-5

Thursday, 6 April 2017

Utii ni bora kuliko sadaka



Habari msomaji wangu,

Karibu kwenye somo la leo.
Tunasoma kutoka kitabu cha Yeremia 34 kinachoongelea jinsi Mungu mwenyenzi alipoongea na nabii Yeremia na kumpa maagizo yake ili awaambie watu wa Yuda wakaao Israeli nini Mungu anapenda wafanye.

Lakini ukiendelea kusoma unaona jinsi wana wa Yuda hawakutaka kutii maagizo ya Mungu bali kufuata mambo ambayo waliyapokea kutoka kwa mababu zao. Hayo mambo  waliyapenda na kuyaamini kuwa yanawasaidia na hivyo kupelekea hasira ya Mungu kuwaka katikati yao na wao kupelekwa utumwani Babeli.

Mungu akawaambia nitawapa uhuru wa kuteswa na mataifa utumwani. Kumbe Yuda walikuwa na ulinzi wa kimungu juu yao ya kuweza kuzuia watu wasiwatese au kuwaonea. Lakini Mungu akaiondoa wakabaki wenyewe bila ulinzi na hivyo wakateseka kwa mapigo mbalimbali.

Je wewe unateseka na mambo gani katika maisha yako? Umewahi kujiuliza kama bado una ulinzi wa kimungu au umeshatoweka? Mara nyingi kukataa maagizo ya Mungu kunapelekea kuondolewa ulinzi katika maeneo ya maisha yako. Unatakiwa kujichunguza na kujihoji kama unafuata kwa uaminifu maagizo yote yaliyoagizwa kwenye neno la Mungu.

Vitu tunavyoagizwa na Mungu kupitia neno lake ni  kupendana, kusameheana, kuinuana, kutoa zaka na sadaka mbalimbali, kusaidia wasiojiweza, kumsifu na kumuabudu, kuishi maisha matakatifu nk.
Ni vizuri kuyafanya haya yote kwa uaminifu. Mtumie Roho mtakatifu nae atakuwezesha kufanya haya. Pia jitahidi kusoma neno la Mungu kwani ndilo uzima na litakuwezesha kujua nini cha kufanya na kwa namna gani. Kumbuka hakuna kinachoshindikana kwa Bwana kama ukiamua na kuamini.

Utii ni Bora kuliko sadaka, kwahiyo nivema ukatii maagizo ya Mungu na hapo ndipo utakapokua chini ya ulinzi wa Mungu katika kuingia kwako na kutoka kwako, na shetani hatapata nafasi katika maisha yako.

Matatizo mengi huja kwa kuachwa mlango wazi katika maisha yako. Funga milango yako yote ili shetani asipate nafasi. Funga milango ya uongo, uvivu, wivu, masengenyo, ulafi, uzinzi, ufisadi, kuabudu/kutegemea miungu mingine n.k. uone kama utaonewa tena na shetani. Hakika hatapata nafasi.

Usiwe kama wana wa Israeli ambao hawakutii maagizo ya Mungu, na mabaya yakawapata. Anza kutii maagizo ya Mungu leo uishi katika ulinzi wake.